Tumaini jipya kwa watoto wenye magonjwa ya moyo: JKCI na China waunganisha nguvu
-
Author: JKCI Admin
-
Published At: Wednesday, Dec 17, 2025
Watoto wa Kitanzania wenye magonjwa ya moyo wanatarajiwa kunufaika na huduma za uchunguzi, matibabu na upasuaji wa moyo bila malipo, kupitia ushirikiano mpya kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Watu wa China unaotekelezwa kupitia Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
Ushirikiano huo ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi ya Rais wa China Xi Jinping aliyoitoa katika Mkutano wa Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) uliofanyika mwaka 2024, akisisitiza kuimarishwa kwa ushirikiano wa sekta ya afya kati ya China na Tanzania.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati viongozi kutoka International Health Exchange and Cooperation Center ya nchini China walipotembelea taasisi hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge alisema Serikali ya China imetuma timu ya wataalamu wa afya nchini kwa ajili ya maandalizi ya andiko la makubaliano ya ushirikiano (MoU), hatua itakayowezesha mpango huo kuanza rasmi mwaka ujao.
Alisema lengo la ushirikiano huo ni kujenga uwezo wa wataalamu wa afya wa Tanzania, kupitia mafunzo na elimu ya juu yatakayowawezesha kufikia viwango vya kimataifa katika matibabu ya magonjwa ya moyo.
“Wataalamu kutoka Serikali ya Watu wa China wamefika JKCI ili kuona kwa vitendo namna ya kuanza ushirikiano huu unaolenga kukuza taaluma za wataalamu wetu wa afya,” alisema Dkt. Kisenge.
Aliongeza kuwa kupitia mpango huo, uchunguzi wa awali wa magonjwa ya moyo utafanyika kwa watoto waliopo mashuleni na wale watakaobainika kuwa na matatizo ya moyo watapatiwa matibabu huku baadhi yao wakifanyiwa upasuaji wa moyo bila gharama yoyote.
Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo alisema mafanikio hayo yametokana na uongozi thabiti wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha huduma za ubingwa bobezi ndani ya nchi hatua iliyoiwezesha Tanzania kuvutia ushirikiano wa kimataifa katika sekta ya afya.
“Kupitia ushirikiano huu JKCI itanufaika kwa kupatiwa vifaa tiba vya kisasa vitakavyotolewa bila gharama, jambo litakaloimarisha zaidi huduma za upasuaji wa moyo nchini na kupunguza rufaa za nje,” alisema.
Aidha Dkt. Kisenge alisema ushirikiano huo utahusisha pia tafiti za magonjwa ya moyo zitakazosaidia kubaini mapema vihatarishi na kulinda afya za wananchi, hususan watoto.
Kwa mujibu wa Dkt. Kisenge, lengo la muda mrefu la ushirikiano huo ni kuifanya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kuwa kituo kikubwa cha rufaa cha matibabu ya moyo barani Afrika na duniani.
Kwa upande wake Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto kutoka Hospitali ya Shandong Provincial iliyopo nchini China ambaye pia anafanya kazi JKCI Zhao Lijian alisema ushirikiano huo ni hatua muhimu katika kuimarisha huduma za matibabu ya moyo kwa watoto barani Afrika hususan Tanzania.
Alisema timu ya wataalamu kutoka China imevutiwa na kiwango cha huduma kinachotolewa na JKCI hali iliyochangia Serikali ya China kuona umuhimu wa kushirikiana na taasisi hiyo ili kuboresha zaidi uchunguzi, matibabu na upasuaji wa moyo kwa watoto bila gharama.
“Ushirikiano huu utawapa wataalamu wa magonjwa ya moyo wa Tanzania fursa ya kubadilishana uzoefu wa kazi, kupata mafunzo ya vitendo na kutumia teknolojia za kisasa za matibabu ya moyo,” alisema Dkt. Zhao.
Aliongeza kuwa hatua hiyo itaongeza uwezo wa ndani na kuhakikisha huduma za ubingwa bobezi kwa watoto zinaendelea kutolewa hata baada ya kukamilika kwa programu ya ushirikiano.
Dkt. Zhao alisema China itaendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Tanzania na JKCI kuhakikisha watoto wanaogundulika kuwa na magonjwa ya moyo wanapata matibabu kwa wakati huku lengo kuu likiwa ni kuokoa maisha ya watoto, kuimarisha urafiki wa muda mrefu kati ya Tanzania na China, na kuchangia maendeleo ya sekta ya afya nchini.